Mhe. Idrissa Kitwana Mustafa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, akiwahimiza viongozi kushuka chini kwa wananchi na kuacha Ofisi zao ili kusikiliza changamoto.
Ameyasema hayo alipokuwa katika muendelezo wa ziara yake katika jimbo la Bumbwini na jimbo la Mahonda Mkoa wa kaskazini Wilaya ya kaskazini B.
Aidha, alisisitiza kuwa yeye ni Waziri wa wananchi na ataendelea kutekeleza maelekezo ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Hussein Ali Mwinyi kwa kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa ufanisi ili iwe ni alama ilioachwa na Serikali yao.
Nae Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Garlos Nyimbo alisema, wananchi watapata fursa ya kuwasilisha changamoto mbalimbali, zikiwemo zinazohusu wizara hiyo inayohusika pamoja na zile zilizo chini ya Mamlaka za Wizara nyingine, Ili kupatiwa ufumbuzi.
Aidha Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini B, Juma Sururu Juma, amewahimiza wananchi ushirikiano katika kutambua vipaumbele vya maendeleo ili kutafutiwa suluhisho la changamoto zinazowagusa moja kwa moja.
Wananchi wa Jimbo la Bumbwini na jimbo la Mahonda walimpongeza Mhe. Waziri kwa uamuzi wake wa kufika kusikiliza kero zao wakieleza kuwa hatua hiyo inaonesha dhamira ya kweli ya Serikali ya kutatua changamoto zinazowakabili.
Mkutano huo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha mawasiliano kati ya Viongozi na Wananchi, pamoja na kuhakikisha changamoto zinazowakabili wananchi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.